Monday, August 24, 2009

Moto mkubwa wateketeza Athens


Maelfu ya wakazi kadhaa wa mji wa Athens nchini Ugiriki wameokolewa katika nyumba zao kufuatia moto wa mstituni unaoendelea kuuzunguka mji mkuu huo.

Karibu watu wote wa Aglos Stefanos, kilomita 23 kutoka kaskazini mashariki mwa Athens, walikimbia moto huo kwa magari au kwa miguu.

Moto umekuwa ukiteketeza eneo la kilomita 50 ukichochewa kwa upepo mkali usiotabirika.

Moto huo ambao ni mkubwa kuliko ule wa mwaka 2007 uliouwa watu 70, unaelezewa kama ni angamizo kwa mazingira.

Juhudi za uzimaji moto zilisimamishwa wakati wa usiku giza lilipoanza kuingia siku ya Jumapili, huku moto huo ukiendelea kuwaka wakati wa usiku, ingawaje hakuna majeruhi walioripotiwa.

Ingawa moto huo umeripotiwa kupungua katika maeneo ya mjini ulikuwa bado unaendelea kuteketeza zaidi maeneo ya misitu.

''Kubadilikabadilika kwa mwelekeo wa upepo kunatabiri moto huo'' msemaji wa kikosi cha zama moto Giannis Kapakis ameliambia shirika la habari la Reuters. ''Ni lazima wote tuwe watulivu katika kipindi cha usiku huu.''

Nyumba kadhaa zimeteketezwa na hali ya hatari imetangazwa katika eneo la mji wa Athens.

Waziri mkuu Costas Karamanlis amesema nchi inakumbana na ''mkasa mzito'' lakini akapongeza juhudi za waokozi kwa juhudi zao za kishujaa.

Italia, Ufaransa na Cyprus zimetuma ndege kusaidiana na vikosi vya zima moto vya Ugiriki.

Polisi wakiwa na vipaza sauti walizunguka katika eneo la Agios Stefanos mapema Jumapili kuwaasa wakazi kuelekea Athens mara moja.

''Tumekuwa tukiomba serikali tangu asubuhi kutuma vikosi'', amesema Panayiotis Bitakos makamu Meya wa eneo hilo. ''Muda umekwisha sasa, umekwisha sana.''

Moto huo unaripotiwa kuwa umeanza siku ya Ijumaa katika eneo lililotengwa kutupa takataka la Grammatiko, karibu na mji mkongwe wa Marathon.

Moto huo unasambaa kwa kasi katika vilima nje ya mji wa Athens, ukiteketeza misitu.

Moto huo uliongezaka zaidi siku ya Jumamosi na kusambaa hadi Varnavas. Hadi siku ya Jumapili asubuhi nyumba zilikuwa zinaungua katika vitongoji vya Athens vya Drafi, Pikermi na Pallini.

Wakati wa usiku moto ulikumba kilele cha Pendeli, katika mwinuko, kitongoji cha kaskazini kinachoonyesha mandhari ya mji wa Athens, ukiteketeza majumba.

Sehemu kubwa ya mlima wa Pendeli iliteketezwa mwaka 2007, anasema Malcolm Brabant aliyeko Athens.

Miti iliyokuwa katika milima mitatu kati ya minne inayozunguka mjii mkuu Athens, ilishateketezwa katika matukio yaliyopita ya moto na mmomonyoko wa udongo katika misitu utakuwa ni wa kutisha, mwandishi wetu anaongeza.

Mkasa mzito

Mamia ya vikosi vya zima moto na wanajeshi vikisaidiwa kwa helikopta na ndege vimekuwa vikidondosha maji toka angani kuzima moto, lakini moto huo ulikuwa mkubwa kupindukia kuweza kudhibiti, mwandishi wetu anasema.

Gavana wa Athens Yiannis Sgouros ameiambia televisheni ya Ugiriki kuwa zaidi ya akari 30,000 za ardhi zimeteketezwa, katika kile anachokielezea kama ni ''maangamizi ya mazingira.''

Wakati wakazi wengi katika maeneo yaliyotishiwa na moto huo walifuata maelekezo ya kuhama, wengine walibaki wakijaribu kulinda nyumba zao.

Moto huo umesababisha moshi mzito katika anga la Athens.

No comments:

Post a Comment